Tuesday, July 23, 2013

Mahakama maalum zitapunguza mlundikano wa wafungwa

Mahakama maalum zitapunguza mlundikano wa wafungwa

Shirika lisilo la Kiserikali linalojishughulisha na mazingira, haki za binadamu na jinsia (Envirocare).

Uanzishwaji wa Mahakama maalumu (zinazohamishika) na watoa msaada wa kisheria katika maeneo ya magereza, kutapunguza mlundikano wa wafungwa.

Ripoti ya hali ya mahabusu za watoto na watu wazima kwenye mikoa mitano ya Tanzania, inaeleza hayo katika utafiti uliofanywa na Shirika lisilo la Kiserikali linalojishughulisha na mazingira, haki za binadamu na jinsia (Envirocare).

Mkurugenzi wa Envirocare, Loyce Lema, alisema ripoti hiyo imependekeza Mahakama zinazohamishika, kutokana na mlundikano wa mahabusi, wengi wakiwa wana kesi ndogondogo.

“Katika magereza 16 na mahabusi za watoto nne, tumegundua wengi wako huko kwa kuwa hawana uelewa wa sheria, wana kesi ndogo ndogo hawastahili kuwapo humo,” alisema.

Mratibu wa mradi huo, ambaye pia ni Naibu Mkurugenzi wa Envirocare, Catherine Jerome, alisema ulianza Septemba, mwaka jana, walitembelea magereza katika mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Morogoro, Tanga na Kilimanjaro.

Alisema lengo la mradi ni kuishauri serikali namna bora ya kupunguza mlundikano wa mahabusi mojawapo ikiwa ni kuwa na wasaidizi wa masuala ya kisheria watakaowaelekeza mahabusi jinsi ya kupata dhamana na haki nyinginezo.

Jerome alisema wametoa mafunzo kwa wasaidizi wa kisheria 88, wawili wenye cheti cha sheria kutoka miongoni mwa maafisa wa gereza na wawili kutoka kwenye jamii jirani na gereza.

Mwasilishaji wa ripoti hiyo kwa wanasheria, watendaji wa Jeshi la Polisi na Magereza katika mkutano wa pamoja kuijadili uliofanyika jijini Dar es Salaam, ambaye pia ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Issai Seng’enge, alisema mahabusi 2,896 walihojiwa.

Alisema katika magereza saba kuna wafungwa na mahabusi wengi kuliko uwezo wa mahakama na wengi hawana uelewa wa masuala ya sheria kwani asilimia 69.42 wana elimu ya msingi na asilimia 84.37 wanatoka kwenye familia za kipato cha chini.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Kennedy Gastorn, alisema kwa Tanzania Bara kuna magereza 122 zenye uwezo wa kubeba watu 29,400, lakini waliopo ni 32,000 na asilimia 51 ni wanasubiri hatima ya kesi zao.


CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment